NA Berensi Alikadi-Bunda
WAFUGAJI wa jamii ya Kitaturu waishio katika Tarafa za Chamliho wilayani Bunda
wamesema kuwa wamechoshwa na vitendo vya manyanyaso wanavyofanyiwa na mwekezaji
wa kampuni ya Grumet.
Wafugaji hao walitoa malalamiko yao hayo juzi kwenye mkutano wa wafugaji hao
katika kijiji cha Maliwanda kwa viongozi wa mashirika matatu yanayojihusisha na
kutetea wafugaji ya Taphgo Shemajawa na Fumuco yenye makao makuu yake katika
mikoa ya Arusha,Dare-salaam.
Wamedai kuwa kwa muda mrefu sasa wamekuwa wakifanyiwa vitendo vibovu na Askari
wa mwekezaji,kampuni ya Grument iliyoko wilayani Serengeti ambayo imemilikishwa
eneo la kawanga ambalo wao walikuwa wakilitumia huko awali kama makazi yao na
malisho yao ya mifugo.
Walivitaja vitendo hivyo kuwa ni pamoja na kuchapwa viboko,kubakwa wakati
wanapoenda kusenya kuni na kutozwa faini kubwa pindi wakamatapo mifugo yao na
kutowapa stakabadhi.
Walisema kuwa pamoja na agizo la serikali alilitoa mwaka jana aliyekuwa waziri
wa mali asili na utalii,Shemsa Mwangunga kuwa wachunge mita mia lakini
mwekezaji huyo amelipuuza na matokea yake asikari wake wamekuwa wakiwanyanyasa
kwa kuwakamata.
”Mimi sifahamu kama huyu mwekezaji na serikali nani ana mamlaka maana kama
waziri mwenye dhamana alikuja hapa na akatuambia kuwa sasa tumeruhusiwa kuchunga
mita mia lakini huyu mwekezaji anatukamata kwakweli tunashangaa sana sijui kama
serikali yetu hii imeshawekwa mfukoni na hawa wazungu”alihoji Mahena Gejera
mkazi wa Maliwanda.
Wafugaji hao walifafanua kuwa askari hao wa mwekezaji wamekuwa wakiwatoza
shilingi laki tano kila wanapokamata mifugo ambapo wamekuwa hawawapi stakabadhi
ya serikali jambo ambalo walihoji kuwa hawafahamu kuwa pesa hizo zinaenda
mikononi mwa mzungu au serikali.
Waliongeza kuwa tayari askari wa mwekezaji huyo wamejenga zizi kubwa eneo hilo
la kawanga na kwamba kila siku lazima wafanye juu chini wakamate mifugo hata
kama inavuka kwenda kunywa maji ili mradi tu wape pesa.
Naye mfugaji mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Sancho Masegenya alieleza kuwa
askari hao wanapo wakamata huwauliza kuwa kama wanatoa shilingi milioni moja
basi wataandikiwa stakabadhi na kwamba kama watatoa shilingi laki tano basi hizo
hawatapewa stakabadhi, hivyo kutokana na uelewa mdogo wa wafugaji hao hulazimika
kutoa pesa hizo ili kunusuru mifugo yao.
Kufuatia manyanyaso hayo wafugaji hao wamedai kuwa sasa wamechoshwa na vitendo
hivyo na kwamba sasa wako tayari kwa lolote lile kwani hata wao wanazo silaha za
jadi hivyo hawaogopi hizo bunduki za mwekezaji.
Wamesisitiza kuwa hawawezi kuendelea kuwa watumwa ndani ya nchi yao kwani wao
kama wafugaji mchango wao ni mkubwa sana katika kuinua uchumi wa taifa hili.
Walipotakiwa kutoa ufafanuzi kuhusu tuhuma hizo afisa mmoja wa kampuni hiyo
ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini alikiri kuwepo kwa taarifa hizo na
akawataka wafugaji hao kutoa taarifa kwa uongozi wa kampuni hiyo pindi mambo
hayo yanapokuwa yanajitokeza.
”Ni kweli malalamiko hayo yapo hata hivi tunapoongea jana kuna watumishi wawili
wamefukuzwa kazi kutokana na mambo hayo na sisi kampuni yetu hairuhusiwi kutoza
watu faini kama hao askari wanafanya hivyo ni makosa tena makubwa.”alisema
afisa huyo.
Naye mwanasheria toka shirika la Taphgo Daud haraka amesema kuwa ni kosa kisheri
kwa askari wa mwekezaji huyo kuwanyanya asa wafugaji hao na kuahidi kulifanyia
kazi suala hilo haraka.
Daudi alisema kuwa nchi hii inaendeshwa kwa misingi ya sheria na kwamba mahakama
pekee ndiyo imepewa mamlaka ya kuhukumu na kutoa haki na wala si vinginevyo
hivyo askari hao wanavunja sheria za nchi kwa kuwabaka akina mama hao wa
Kitaturu na kwamba jambo hilo halitafumbiwa macho.
mwisho